
Wajumbe wa Bunge la Katiba wakiomba kabla ya kuahirishwa kwa Bunge mjini Dodoma juzi. Picha na Silvan Kiwale
Dodoma. Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) sasa upo hatarini kufutwa kutokana na kutuhumiwa kutumika kuwachochea wajumbe kufanya vurugu katika Bunge la Katiba.
Mwenyekiti wa Bunge hilo, Samuel Sitta aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa hata jina la umoja huo la Umoja wa Katiba ya Wananchi ni la “kiburi” na linalenga kuonyesha ni wao pekee ndio wanaotetea wananchi, kitu ambacho mwenyekiti huyo alisema siyo sahihi.
Hata hivyo, mwenyekiti wa Ukawa, Freeman Mbowe alikanusha tuhuma kuwa umoja huo unafanya vurugu na kusisitiza wataendelea kutetea hoja za wananchi katika Rasimu ya Katiba hadi mwisho.
“Kwanza hoja hii ya katiba mpya kwa muda mrefu inatokana na vyama vya upinzani, mashirika yasiyo ya kiserikali (NGOs) na wananchi. Sasa haiwezekani tukavuruga kupatikana katiba bora. Sisi tutaendelea kutetea maoni ya wananchi ya kupata Katiba bora hadi mwisho,” alisema Mbowe.
Ukawa kupelekwa Kamati ya Kanuni na Haki za Bunge
Sitta alisema wamechoka kuvumilia vitendo vya umoja huo hivyo watapeleka malalamiko kwenye Kamati ya Kanuni na Haki za Bunge na pia serikalini ili kuona namna ya kufanya.
“Tunafuatilia vikao vyao vyote, kuna mambo wanazungumza ni ya kusababisha vurugu, ngoja niwasomee hapa. Wanasema ‘hakuna haja ya kujitoa bungeni, ikiwa masilahi ya Ukawa hayajatekelezwa ikiwepo uteuzi wa wajumbe basi hatatoka mtu bungeni’,” alinukuu taarifa hiyo.
Alisema pia kikao cha Ukawa, kilipendekeza Kamati ya Uongozi lazima ifumuliwe yote na pia wateuliwe wajumbe kutoka Ukawa na kuwepo uwiano wa Muundo wa Muungano katika kamati.
“Kumbuka hawa watu hawakujitokeza kugombea baada ya kupatikana watu wa CCM wanasema sasa kamati ifumuliwe, wanazusha mambo mapya, lazima uwepo usawa katika kamati. Huku ni kuleta fujo,” alisema Sitta. Alisema katika uchaguzi wa Kamati ambazo CCM ilipata ushindi katika kamati nyingi, wajumbe wa Ukawa hawakugombea, isipokuwa Profesa Ibrahimu Lipumba pekee, ambaye alishindwa na Anna Abdalah.
“Sasa wanasema ikiwa Sitta hataki kututeua basi hakuna biashara ambayo itafanyika bungeni na hatoki mtu bungeni. Hii sio sawa,” alisema.
Ukawa ni Umoja wa Katiba ya Wananchi ambao unaundwa na wajumbe 286 wengi wao wakiwa ni wabunge wa upinzani na makundi mengine yaliyoteuliwa na Rais.
Jakaya Kikwete.
src
mwananchi
src
mwananchi