Wednesday, February 19, 2014

Kamati Kuu CCM ilikesha Dodoma kuwasulubu vigogo


Dar es Salaam. Kamati Kuu ya CCM ilikesha katika kikao kilichofanyika usiku wa kuamkia juzi, ambacho kiliwapa adhabu ya kuwa chini ya uangalizi wa miezi 12, vigogo sita, baada ya kuwatia hatiani kwa makosa ya kuanza mapema kampeni za kuusaka urais wa 2015 kabla ya muda uliowekwa na chama hicho.

Vigogo hao ni Mawaziri wakuu wa zamani, Edward Lowassa na Frederick Sumaye, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Stephen Wassira, Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba na aliyewahi kuwa Waziri wa Nishati na Madini, WilliamNgeleja.

Habari ambazo zimelifikia gazeti hili zinasema Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete katika hali isiyotarajiwa, aliongoza kikao cha Kamati ya Maadili, kilichofanyika muda mfupi baada ya kuzungumza na wajumbe wa CCM katika Bunge Maalumu la Katiba.

“Mwenyekiti (Rais Kikwete) baada ya kumaliza mazungumzo na wabunge alitarajiwa kuondoka kwenda Dar es Salaam lakini kwa mshangao, tuliambiwa ana kikao hivyo magari yaliyokuwa yamewekwa tayari yalirudishwa kwenye maegesho yake,” kilisema chanzo chetu kilichopo Makao Mkuu ya CCM Dodoma.

Habari zaidi zinasema wakati Rais Kikwete akiongoza kikao hicho ambacho kilipokea taarifa ya Kamati ndogo ya Maadili, aliagiza Kamati Kuu iitishwe saa 2:00 usiku. Kikao hicho cha Kamati Kuu kiliendelea hadi usiku wa manane.

“Hata sisi hapa makao makuu ni kama hatukuwa tukifahamu kilichokuwa kikiendelea, lakini ilipofika kama saa 2:40 hivi Kamati Kuu ilianza na kubwa lilikuwa ni kuhusu hatua za kinidhamu kwa hao wakubwa (vigogo),” kiliongeza chanzo hicho.

Hata hivyo, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alisema jana kuwa, vikao hivyo ni vya kawaida kwani matokeo ya kazi ya Kamati Ndogo ya Maadili iliyoongozwa na Makamu Mwenyekiti wa CCM – Tanzania Bara, Philip Mangula ilipaswa kuwasilishwa katika vikao hivyo.

Wafuasi wachelea

Uamuzi huo wa kuwapa onyo kali vigogo hao, ni dhahiri umewatisha baadhi ya viongozi wa chama hicho ambao walishatangaza kuwaunga mkono baadhi ya wagombea, kwani wengi walipotafutwa jana walisita kuzungumza.

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga, Khamis Mgeja alipoulizwa kuhusu hatua hiyo alisema uamuzi wa vikao vya chama hicho hupokewa bila kupingwa kama zilivyo amri za kijeshi na kinachofuata ni utekelezaji. Mgeja alisema kama vikao vimeamua hivyo hana cha kuongeza.

Mgeja, Mbunge wa Mbinga Magharibi, John Komba, Mwenyekiti wa CCM, Mkoa wa Singida, Mgana Msindai na Mbunge wa Kilindi, Beatrice Shelukindo kwa nyakati tofauti, walishatangaza kumuunga mkono Lowassa atakapowania urais katika Uchaguzi Mkuu wa 2015.

Msindai kwa upande wake alisema kama vikao vilivyokaa kuwaonya Lowassa na wenzake vilifuata katiba ya chama hicho basi wanastahili adhabu hiyo lakini kama vilikosea hiyo ni hatari kwa chama.

“Sijasoma katiba na kuunganisha uamuzi huo wa Kamati Kuu. Kama wamefuata katiba kutoa uamuzi wao hakuna tatizo, ila tatizo litakuja kama hawajafuata katiba ya chama kuwaadhibu.”

Alipoulizwa Komba alisema: “Niko bungeni siwezi kulizungumzia suala hilo,” huku Shelukindo akisema bado hajafuatilia kwenye vyombo vya habari kuhusu onyo hilo na kwamba atatoa maoni yake marabaada ya kusoma.

Hata hivyo, Katibu wa Uhamasishaji na Chipukizi wa Umoja wa Vijana (UVCCM), Paul Makonda alisema kitendo cha Kamati Kuu kuwajadili vigogo hao kinaleta matumaini kwa wanachama wanaokitakia mema chama hicho... “Kunaonyesha kwamba hakuna mtu aliye juu ya sheria, kanuni na taratibu katika chama.”

Hata hivyo, Makonda alishangazwa na Kamati Kuu kutoa adhabu sawa kwa wanachama wote sita akisema haiwezekani kuwa wote walifanya makosa sawa katika mazingira yanayofanana

 src-mwananchi