Monday, May 12, 2014

WABUNGE, NINI FAIDA YA RIPOTI YA MKAGUZI MKUU KAMA HAMFANYII KAZI?


Nianze kwa kumuomba Mungu atuzidishie amani katika nchi yetu huku akitupa afya njema ili tuweze kumtukuza na kumsifu daima kwa wema wake kwetu.
Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Bw. Ludovick Utouh.
Baada ya kusema hayo niingie katika mada ya leo ambapo nitazungumzia ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ya mwaka wa fedha wa 2012/13 iliyofichua madudu ya ajabu, ambayo bila shaka yatakuwa yameondoa matumaini ya wananchi ya kukua kwa uchumi na kuwaondolea umaskini uliokithiri.
Ni kawaida kila mwaka ripoti za CAG ya ukaguzi wa fedha za umma huwa zinafichua mambo mazito ya ubadhirifu wa pesa za serikali lakini hakuna hatua zinazochukuliwa ili iwe fundisho kwa watu wanaotafuna fedha hizo kama mchwa.
Lakini ni jambo la kusikitisha kwamba ripoti iliyotolewa ufafanuzi na CAG mwenyewe, Ludovick Utouh  wiki iliyoopita mjini Dodoma imeonyesha dhahiri kwamba serikali haijawa na dhamira ya kweli ya kudhibiti matumizi haya mabaya ya fedha za umma na kupambana na vitendo vya ufisadi na ubadhirifu wa mali za nchi.
Tunajua kuwa lipo Bunge na mifumo mingine kadhaa ya umma ya kuhakikisha kwamba serikali inakuwa na nidhamu katika kusimamia mapato na kudhibiti matumizi yake, bado hakuna mabadiliko wala dalili za uwajibikaji katika matumizi ya fedha hizo za umma nchini.
Ripoti ya CAG inaonyesha kwamba matumizi hayo mabaya yanaendelea kufanywa na maofisa wa serikali pamoja na hali mbaya ya uchumi inayolikabili taifa. Kwa mwenendo huo, inaonekana hakuna uwezekano wa kupunguza Deni la Taifa ambalo tumeambiwa limefikia shilingi trilioni 21.20, ambalo ni ongezeko la shilingi trilioni 4.23 sawa na asilimia 25, ikilinganishwa na shilingi trilioni 16.98  katika mwaka wa fedha wa 2011/12.
Ndani ya serikali umekuwamo utamaduni wa ufujaji wa fedha za serikali  ambao umechangia kupanda kwa deni la ndani kutoka shilingi trilioni 4.55  mwaka 2011/2012 hadi shilingi trilioni 5.78 mwaka wa 2012/13, likiwa ni ongezeko la shilingi trilioni 1.23, sawa na asilimia 27.
Haya ni mambo mazito ambayo mwananchi wa kawaida ni vigumu kwake kuyajua lakini wabunge ambao ndiyo wasimamizi wa serikali, watakuwa ni waajabu sana kama watakaa kimya wakati ubadhirifu huu unafanywa na wenzetu wachache tuliowapa dhamana ya kutuhudumia.
Mwenendo huo ni hatari kwa uchumi na maendeleo ya taifa letu. Baya zaidi ni pale serikali inapoendekeza mikopo kutoka katika benki za biashara nje ya nchi.
Ripoti ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT), inasema kwamba serikali imekuwa ikikopa wastani wa shilingi bilioni 360 kwa mwezi kutoka nje. Kutokana na hali hiyo, Shirika la Fedha Duniani (IMF) na Benki ya Dunia (WB), vimeonya dhidi ya mwenendo huo kwamba utahatarisha uchumi wa nchi.
Miradi mingi ya maendeleo imekuwa ikikwama kutokana na fedha zake kuingizwa katika michepuko isiyofaa, mbali na wizi na ubadhirifu wa baadhi ya wanasiasa, watendaji wa serikali na taasisi zake.
Ripoti ya CAG imebaini ufisadi mkubwa katika maeneo mengi ya mapato na matumizi ya fedha za serikali.
Kwa mfano, magari mapya 11 yenye thamani ya mamilioni ya shilingi yalinunuliwa lakini anasema yaliishia katika miliki za watu binafsi. Mdhibiti wa fedha za serikali anasema hayo lakini Bunge linakaa kimya, sasa kuna faida gani mzee Ludovick na timu yake kuwafanyisha kazi isiyozaa matunda?
Katika ripoti yake anasema mamilioni ya shilingi yalitumika kulipia mishahara kwa watumishi hewa, hili nalo kweli linafumbiwa macho au mpaka amri itoke kwa rais wa nchi?
Kama hilo halitoshi tukaambiwa kuwa kuna misamaha ya kodi ambayo imefanya taifa likose mapato ya shilingi trilioni 1.52!
Hizi ni fedha nyingi sana. Wabunge mnakaa kimya bila kujua kuwa fedha hizo zingeweza kujenga shule za sekondari za kisasa zaidi ya 300 nchini, nini faida ya ukaguzi wa CAG?.
Nilitegemea baada ya ripoti ya CAG wabunge wangeungana kutaka waliofanya ubadhirifu huo wa fedha za umma kuwajibishwa lakini ajabu sijasikia ukemeaji wowote. Wananchi siyo vipofu, wanaona kinachofanyika.
Jipu limepasuka, siwezi kuwa adui kwa kusema ukweli.


src
GPL