UPATIKANAJI wa damu ya kutosha iendayo kwenye uume na ucheleweshwaji wa damu kurudi, vitu hivi viwili vinahitajika ili uume ufanye kazi ya kusimika. Magonjwa yanayosababisha kufanya ateri za mishipa ya damu kuwa myembamba na kupunguza damu kwenda kwenye uume (kama mishipa ya damu kuwa migumu, hupunguza uwezo wa kunyumbuka kama ilivyo kwa ugonjwa wa kisukari, kuwa na damu iliyoganda).
Kama mtu atafanyiwa upasuaji huenda damu ikachelewa kufika mahali inapohitajika kwa wakati, tatizo hilo sio la kudumu na baada ya muda hali inajirudia kuwa nzuri.
Agizo analopewa mgonjwa anapofanyiwa upasuaji katika sehemu zinazohusiana na eneo nyeti la mwanamume, huelezwa asubiri kwa miezi mitatu au sita kabla hali ya kutenda tendo la ndoa, ili apate nafuu ya kumudu kile anachokusudia kufanya. Wanaume wengine huzaliwa na kasoro za mfumo wa mishipa ya damu katika sehemu ya siri inayohusika.
Hali kama hiyo ambayo itaathiri upelekaji wa damu huweza kuleta upungufu wa nguvu za kiume.
Ni vema yeyote anayehisi kwamba nguvu zake za kiume zina kasoro, anashauriwa amuone daktari achunguzwe kuliko kuvamia dawa ambazo zinaweza kuleta athari kubwa kuliko kile ulichokitegemea.
Mishipa ya fahamu ya ubongo na ile iendayo kwenye uti wa mgongo inapoathirika inaweza kusababisha upungufu wa nguvu za kiume. Mshipa wa fahamu/neva uendao au unaotoka kwenye sehemu za siri za mwanamume, unapoathirika kwa ugonjwa au ajali ni sababu mojawapo inayoweza kuleta upungufu wa nguvu za kiume.
Wanaopata ajali za kuanguka kwenye mashimo na vyoo visivyofunikwa, au wanaoumia kwenye pikipiki au baiskeli kwenye sehemu za msamba wanaweza kuharibu mishipa yao ya fahamu/neva na hatima yake endapo hatapata tiba stahili anaweza kupata upungufu wa nguvu za kiume.
Si kawaida lakini, usiogope kufanyiwa upasuaji wa tezi dume endapo utakuwa na saratani au uvimbe kwenye tezi dume moja ya athari tokezi ni kupungua nguvu za kiume.
Faida utakayoipata kwa kufanyiwa upasuaji huo ni kubwa na ya manufaa kwa mteja ukilinganisha na kupungua nguvu za kiume.
Uharibikaji wa mishipa ya fahamu/neva itokayo au iendayo kwenye sehemu za siri za mwanamume kwa magonjwa yafuatayo husababisha upungufu wa nguvu za kiume, kisukari (diabetes) kiharusi (stroke) kinaweza kusababishwa na Virusi Vya Ukimwi (VVU), Ugonjwa wa kifua kikuu (TB) inapoathiri mishipa ya fahamu ya ubongo, uvutaji wa sigara na ulaji wa kuberi, unusaji wa ugoro na ubwiyaji wa mazao yote ya tumbaku, unywaji wa pombe vitu vyote hivyo husababisha upungufu wa nguvu za kiume na huleta madhara lukuki kwa mwili wa binadamu, zikiwemo saratani za viungo mbali mbali.
Kuna baadhi ya dawa mgonjwa anapozitumia anaweza kupata upungufu wa nguvu za kiume. Endapo utumiaji wa dawa hizo utakuepusha na kupata ugonjwa wenye matatizo mengine makubwa zaidi kuliko shida za ugonjwa wa awali, ni vema ukapata wewe mgonjwa kwa uelewa wako na utashi wako kipi kitakupa nafuu.
Gharama za chini kwa kumhudumia mgonjwa mwenye kiharusi aliyeko nyumbani au hospitalini kwa mwezi ni shilingi za kitanzania laki 6 (600,000/-), mwenye ngazi ya juu kimaisha kama Mtendaji Mkuu (Chief Executive Officer) gharama za kumhudumia mgonjwa mwenye kiharusi kwa mwezi ni milioni moja na laki tano (1,500,000/-).
Utakapokacha dawa za shinikizo la damu kuwa huleta upungufu wa nguvu za kiume, je utakuwa tayari kukubali kupata kiharusi? Ninawashauri wagonjwa wote wenye magonjwa ya kusendeka, magonjwa sugu (chronic diseases) kama presha (shinikizo la damu), saratani (cancer-kansa) kifua kikuu, Ukimwi, tafadhali msiache kutumia dawa mpaka pale mtakapopata ushauri wa daktari mhusika anayekutibu.
Athari tokezi (side effects) za dawa zote ni somo linalohitajika mgonjwa, mtoa huduma-tabibu-muuguzi na yule aliyekaribu nawe akupe unasihi, faraja, maelekezo na ushauri nini kifanyike, unapopata hali ya kusononeka (depression) na msongo wa maisha (stress).
Nimezungumzia kuhusu upungufu wa nguvu za kiume, ieleweke bayana kuwa hata mwanamke anaweza kupata upungufu wa nguvu za kike kutokana na unywaji wa pombe za aina yoyote ile. Pombe zile anazokunywa mwanamke pia huathiri siku zake za mwezi (hedhi) ikawa haina mpangilio maalumu.
Uvutaji wa sigara vile vile na magonjwa yote anayopata mwanamume kwa kiwango fulani kwa mwanamke pia hutokea. Katika wanaume wengi niliofanikiwa kuwashawishi waache kuvuta sigara na kunywa pombe ni wakati nilipogusia kuwa:
unywaji wa pombe na uvutaji wa sigara hupunguza nguvu za kiume, hapo ndipo somo lilipoeleweka. Wengi waliacha, na walitoa pongezi kuwa sasa mambo nyumbani ni kama zamani.
Sababu nyingine kubwa inayoleta udhia katika wanandoa na wengine leo wamekimbiwa na wake zao, ni wanaume wanaotumia mirungi-miraa, ambayo hutafunwa kama majani mithili ya mbuzi anayekula majani. Mirungi hiyo huliwa na sukari, chai ya tangawizi au soda ya cola.
Miraa pia huleta magonjwa ya akili kwa jamii wanaotumia miraa kama moja ya tabia na desturi za mahali wanapoishi. Miraa imepigwa marufuku Kenya.
Tanzania miraa ipo na inalimwa na kuvunwa na huliwa na kutafunwa na madereva wa masafa marefu kuepusha usingizi. Haisaidii na wengine hupata ajali kwa kukosa usingizi. Upungufu wa nguvu za kiume pia unaletwa na matatizo ya kisaikolojia hususan kwa vijana wasomi na wale nguvu kazi, na wale pia wasio na kazi.
Masuala ya kisaikolojia ni pamoja na sonona (depression) wasiwasi na woga wa kutenda vizuri, vitu hivyo vyote vikichanganywa kwa pamoja husababisha uume kutosimika na nguvu za kiume hupotea na au hupungua. Masuala ya kisaikolojia yapo kwa kiwango kikubwa kwa vijana wengi.
Chochote kipya katika maisha ya kila siku ambacho huweza kuleta msongo wa maisha (stress), kama kuwa na rafiki mpya katika penzi, au masuala ya kimapenzi kazini haya pia huchangia katika suala la kupungua kwa nguvu za kiume
src
Habari Leo