Tuesday, April 15, 2014

Bunge la #Katiba kuahirishwa kabla ya maadhimisho ya #Muungano [VIDEO]

Dodoma. Bunge Maalum la Katiba linatarajiwa kuahirishwa Ijumaa ijayo, kabla ya maazimisho ya Miaka 50 ya Muungano hapo Aprili 26. Mwenyekiti wa Bunge hilo Samuel Sitta amesema kuwa Aprili 25 itakuwa siku ya mwisho ya majadiliano kwa kipindi hiki cha kwanza ili kupisha Bunge la Bajeti. “Tunapokwenda kwenye sikukuu ya Muungano, ndiyo itakuwa siku ya mwisho kwa ngwe hii hadi tutakapokutana tena mwezi wa nane,” alisema Sitta. Muungano huo wa Tanganyika na Zanzibar wa 1964, uliodumu nusu karne hadi sasa, ni kati ya masuala yaloleta utata na kuibua majadiliano makali katika Bunge Maalum. Kwa takribani wiki tisa sasa, Watanzania wamekuwa wakitazama wajumbe wa Bunge Maalum wakikwaruzana vilivyo kuhusu hatma ya Muungano na mfumo wa serikali katika Katiba Mpya. Mdahalo huo umeendelea kutawala mjini hapa leo, huku wajumbe wengi toka Kundi la Walio Wengi ambalo linaundwa kwa kiwango kikubwa na wana-CCM, wakikazia msimamo wa serikali mbili katika Muungano. Wale Walio Wachache, hasa kutoka vyama vya upinzani na makundi maalum katika Bunge hilo, wameendelea kudai mfumo wa Shirikisho litakaloundwa na serikali 3 katika Katiba Mpya, kama ulivyopendekezwa katika Rasimu ya 2 ya Katiba Mpya.

src Mwananchi